Mfanyabiashara
maarufu, jijini Dar es Salaam, Marijani Msofe 'Papa Msofe', akiongozwa
na Askari Polisi na Magereza kuingia kwenye chumba cha Mahakama ya
Kisutu kwa ajili ya kusomewa shitaka la mauaji ya Onesphory Kitoli,
mahakamani
WAKATI Kesi inayomkabili mfanyabiashara maarufu, Abubakar Marijani
‘Papaa Msofe ikiendelea katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Mfanyabiashara mwingine maarufu Alex Massawe aliyekuwa akisakwa na Askari wa Polisi Afrika Kusini amekamatwa.
Mfanyabiashara
huyo aliwekewa mtego na Polisi wa Afrika Kusini ambao wamekuwa
wakimsaka baada ya kuombwa na Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na Shirika la Polisi la Kimataifa (Interpol) ili akamatwe na kurejeshwa nchini.
Mfanyabiashara huyo anatuhumiwa kwa kosa la mauaji baada ya kutajwa
mahakamani Aprili 4, mwaka huu katika kesi ya mauaji ya mfanyabiashara
Onesphory Kituly ambaye aliuawa katika mazingira ya kutatanisha Novemba
6, 2011 akiwa nyumbani kwake Magomeni, Dar es Salaam.
Katika kesi hiyo ambayo mshtakiwa wa kwanza ni mfanyabiashara maarufu,
Abubakar Marijani ‘Papaa Msofe’, mshitakiwa mwingine, Makongoro Joseph
Nyerere alitoa malalamiko, mbele ya Hakimu Mkazi, Agnes Mchome mara
baada ya Wakili wa Serikali, Mwanaisha Kombo kudai upelelezi wa kesi
hiyo bado haujakamilika na kuomba tarehe mpya ya kuitaja.
Chanzo cha habari hii kutoka ndani ya Jeshi la Polisi Tanzania
ililipasha gazeti moja la kila siku nchini Tanzania kwamba “Unajua kuna
mlolongo wa taratibu za kutekeleza ili Massawe akamatwe. Kwanza lazima
Polisi wa Tanzania watoe tangazo kwa Interpol juu ya kumsaka mtu huyo
ili aletwe. Ndiyo maana Polisi wa Tanzania hawawezi kuzungumza chochote
hadi watakapomweka mikononi mtuhumiwa huyo,” kilieleza chanzo cha gazeti
hilo.
Hata hivyo habarimpya.com imehabarishwa
na vyanzo vya ndani ya Jeshi hilo kwamba pamoja na madai kukamatwa kwa
mfanyabishara huyo nchini Afrika Kusini bado hawezi kuletwa nchini kwa
sasa mpaka serikali ya Tanzania na Afrika Kusini zitakapo toa kibali cha
kusafirishwa kwake.



