Blogger Widgets

Social Icons

Pages

Monday, April 29, 2013

Mjane wa Mwangosi kupewa Sh milioni 10

MJANE wa aliyekuwa mwandishi wa habari wa kituo cha Chanel Ten, marehemu Daudi Mwangosi, Itika Mwangosi anatarajia kukabidhiwa Sh milioni 10 kama kifuta machozi. Itika, atakabidhiwa fedha hizo katika maadhimisho ya siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani, yatakayofanyika jijini Arusha kuanzia Mei 3 hadi 5, mwaka huu. 

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi, Tumaini Mwailenge alisema fedha hizo, zitamsaidia mjane huyo kuanzisha miradi atakayoona inamfaa katika maisha yake.
Alisema mbali ya fedha hizo, utazinduliwa mfuko maalum utakaojulikana kwa jina la Daudi Mwangosi Fund, ambao utakuwa unasaidia kila mwandishi pale anapopata matatizo.
“Mtakumbuka Septemba 2, 2012 mwandishi wa kituo cha Chanel Ten, marehemu Daudi Mwangosi aliuawa katika Kijiji cha Nyololo, wakati polisi wakipambana na wafuasi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).
“Sasa tumeona ni vema tukatoa kifuta machozi kwa mjane wa marehemu Mwangosi, ili aweze kuanzisha miradi yoyote ya biashara na katika maadhimisho ya mwaka huu tutazindua mfuko maalum wa kusaidia waandishi,” alisema.
Alisema maadhimisho hayo, yataadhimishwa ngazi ya Afrika Mashariki, ambapo nchi zote tano zitajumuika pamoja jijini Arusha.
Alisema mada zitakazojadiliwa katika maadhimisho hayo, ni usalama na mazingira bora ya waandishi wa habari Afrika Mashariki, maboresho na mabadiliko ya vyombo vya habari juu ya utendaji kazi.
Nyingine ni haki za binadamu kwa waandishi wa habari nchini Tanzania na hatua zinazochukuliwa na Serikali.
Alisema baada ya majadiliano hayo, litapitishwa azimio la pamoja la waandishi wa habari Afrika Mashariki na kuongeza kwamba kauli mbiu ya mwaka huu ni usalama wa mwandishi wa habari sehemu ya kazi.
Alisema mgeni rasmi katika maadhimisho hayo ni Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Dk. Richard Sezibera.
Katika mkutano wa jana, wawakilishi kutoka vyama vya waandishi wa habari na taasisi walihudhuria na kuzungumzia hali ya usalama wa mwandishi na mazingira yake ya kazi.
Baadhi ya vyama hivyo ni Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC), Baraza la Habari Tanzania (MCT), Jukwaa la Wahariri (TEF), Umoja wa wanahabari wa kimataifa na Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Dar es Salaam (DCPC).
Nyingine ni Taasisi ya Vyombo vya Habari Kusini mwa Afrika Tawi la Tanzania (MISA TAN) na Jukwaa la Katiba Tanzania (JUKATA).

habari NA BENJAMIN MASESE, DAR ES SALAAM
Picha - chingaone  library
chanzo - mtanzania
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...