8724460544_80b0eae728_z
Balozi Leslie Rowe kutoka ofisi ya Serikali ya Marekani anayeshughulikia mambo ya afya.(Picha na Maktaba).
Na Anna Nkinda – Maelezo
 Serikali ya Marekani kupitia  Mpango wa dharula wa kupunguza makali ya VVU  na Ukimwi (PEPFAR) imeipatia Serikali ya Tanzania dola za kimarekani millioni tatu fedha ambazo zitatumika kuwapima na kuwatibu wanawake wanaosumbuliwa na matatizo ya saratani  ya mfuko wa kizazi.
Hayo yamesemwa jana na Balozi Leslie Rowe kutoka ofisi ya Serikali ya Marekani anayeshughulikia mambo ya afya wakati akiongea na watu mbalimbali walioshiriki mkutano wa wake wa Marais wa Afrika uliofanyika katika hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam.
Aidha Serikali ya Marekani pia imetoa  mashine 16 za cryotherapy ambazo zitatumika kama sehemu ya matibabu kwa ugonjwa wa saratani ya mfuko wa  kizazi katika Hospitali ya Kansa ya Ocean Road.
Balozi Rowe alisema  kuwa upatikanaji na mashine hizo  utawasaidia wanawake  wengi ambao wanasumbuliwa na ugonjwa wa Kansa ya shingo ya kizazi kuweza  kupata huduma ya vipimo  na matibabu mapema na haraka.
“Kutokana na maambukizi ya VVU wanawake wengi wako katika hatari kubwa  ya kupata ugonjwa wa saratani ya shingo ya kizazi na matiti  kwa kushirikiana na PEPFAR tutaendelea kuwaunga mkono utepe wa pink,utepe mwekundu kuokoa maisha  ya wanawake.
Jitihada za pamoja  zinahitajika kwa kushirikiana na vikundi vya kijamii na kuimarisha miundombinu ili  kuhakikisha kuwa tunatoa vipimo na matibabu ya saratani kwa wakati”, alisema Balozi Rowe.
Alisema kuwa uongozi wa Rais Obama umeridhishwa na Serikali ya Tanzania kwa jinsi unavyolishughulikia tatizo la saratani  ya shingo ya kizazi na utaendelea kuwaunga mkono wanawake na wasichana Duniani kote ikiwa ni pamoja na katanua program mbalimbali na kutoa fedha  kwa ajili ya elimu, maendeleo ya kilimo na afya.
Akiongea na waandishi wa Habari mara baada ya kumalizika kwa mkutano huo Mama Kikwete aliishukuru Taasisi ya Bush kwa kufanya mkutano huo nchini na kusema kuwa mambo yaliyojadiliwa ni upatikanaji wa elimu kwa mwanamke, upatikanaji wa Afya bora na kumuwezesha mwanamke kiuchumi.
Mama Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA) alisema kuwa mwanamke ni mtu muhimu sana katika jamii haijalishi ana elimu kiasi gani yeye ni mlezi wa familia na  ukimwezesha mwanamke kielimu ni ukombozi mkubwa katika jamii kwani ni rahisi kwake kukabiliana na magonjwa mbalimbali ikiwemo saratani ya shingo ya kizazi.
“Miaka ya nyuma kutokana na baadhi ya watu kutokuwa na elimu ya kutosha kuhusu ugonjwa wa Ukimwi waliweza kuamini kuwa mtu akiwa na maambukizi ya ya VVU amerogwa lakini  hivi sasa baada ya watu kupata elimu wkamekuwa na uelewa mkubwa.
“Ukimwezesha mwanamke kielimu na kiuchumi anakuwa na uhuru wa  kufanya mambo yake bila ya kutegemea msaada kutoka kwa mme wake ninachowaomba wanawake wenzangu mfanye  kazi kwa bidii kwani mwanamke  akiwa na kipato cha  kutosha hawezi kudharaulika”, alisema Mama Kikwete.
Alisema kuwa zamani wanawake wasiokuwa na kazi walikuwa wanaitwa magoli kipa ingawa  walikuwa na kazi kubwa ya kuangalia familia na jamii ikasahau kuwa wanawake ndiyo wazalishaji mali. Pia aliwaomba wanawake wasiogope kuchangamkia fursa zinazopatikana  na wasiache kumuunga mkono mwenzao pale anapoomba nafasi ya kupata fursa hizi  kwani wakiwa pamoja wanaweza.
Katika mkutano huo pia Rais Jakaya Mrisho Kikwete na Rais wa zamani wa Marekani  George Bush walitambulisha rasmi  Utepe wa Pinki , Utepe mwekundu  ambayo ni alliance inayofanya  kazi ya kupambana na kansa ya saratani ya mfuko wa kizazi na saratani ya matiti  katika nchi za Kusini mwa jangwa la Sahara na Amerika ya Kusini.
Tanzania  ni nchi ya tatu Barani Afrika kutambulisha  Utepe wa Pinki , Utepe mwekundu  alliance nchi zingine ni  Zambia na Botswana.
Mkutano huo wa siku mbili  uliomalizika jana  uliandaliwa na Taasisi ya Rais mstaafu wa Marekani George Bush na kuhudhuriwa na baadhi ya wake Wa Marais wa Afrika na Mke wa Waziri mkuu mstaafu Wa Uingereza Cherie Blair.