WAKATI wawekezaji wakigeni wakizidi
kunufaika huku watanzania wakiendelea kuishi katika lindi la
umaskini,Mwenyekiti Mtendaji wa Makampuni ya IPP Media Reginald Mengi
ameipongeza Serikiali ya Rais Jayaka Kikwete kwa hatua ya kuuza nchi
kwa wawekezaji hao.
Pongezi za Mengi kwa Serikali ya Rais Kikwete imekuwa na tafsiri
tofauti kutokana na jinsi ambavyo wawekezaji hao wananufaika kupitia
migongo ya watanzania maskini na rasilimali zao, huku Rais Kikwete na
Serikali yake ikiendelea kulifumbia macho suala hilo.
Mengi ambaye ni miongoni mwa watanzania wachache wanaotumia sehemu ya
mali zao kuwasaidia watanzania wenye maisha magumu hususan walemavu wa
viungo na ngozi, alitoa pongezi hizo kupitia akaunti yake ya Twitter.
"Hongera Tz kwa kuwa labda nchi ya kwanza duniani kubinafsisha
mashirika ya umma na kunufaisha wawekezaji wageni badala ya
wananchi"alitweets Mengi katika akaunti yake.
Kauli hiyo ya mengi pia imekuja ikiwa ni wiki moja tu tangu wananchi
wa Mtwara wafanye vurugu kubwa zilizosababisha vifo vya watu wawili
na kufanya uharibufu mkubwa wa mali.
Vurugu hizo za wanamtwara zilikuwa
na lengo la kupinga hatua ya Serikali ya Rais Kikwete kusafirisha Gesi
kutoka mkoani humo hadi jijini Dar es Salaam na hatimaye kufika Mkoani
Pwani hasa katika Wilaya ya Bagamoyo mahali alipozaliwa Rais huyo.
Kauli ya Mengi pia imekuja katika kipindi ambacho Tanzania inatarajia
kupokea ugeni mkubwa katika historia ya nchi hii. Rais wa Marekani
Barack Obama anatarajia kutembelea Tanzania mwanzoni mwa mwezi Julai
mwaka huu, akiwa na msafara wa watu 700 wenye lengo la kuja kuwekeza
Tanzania.
Ziara hiyo ya Obama inakuja ikiwa ni miezi minne tangu Rais
wa Jamhuri ya watu wa China Xi Jinping alipotembelea Tanzania kwa ziara
kama hiyo ya Obama...