Blogger Widgets

Social Icons

Pages

Friday, July 12, 2013

Matokeo kidato cha 5 yachefua wadau


MATOKEO mabaya ya kidato cha 5, yaliyotangazwa juzi na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, yamezidi kuibua mambo katika sekta ya elimu. Hatua hiyo, imetokana na Serikali kutangaza nafasi 10,000 zimeshindwa kupata wanafunzi kutokana na kufeli masomo yao. Kutokana na hali hiyo, baadhi ya wadau wa elimu wamesema kama Serikali haitachukua hatua za haraka za kunusuru sekta ya elimu nchini, kwa kuboresha mifumo, itarajie anguko kubwa mwaka ujao.

Wakizungumza na MTANZANIA jana, wadau hao walisema mchawi wa anguko la elimu si wanafunzi, bali ni serikali yenyewe, kwa kuwa haijaweka mazingira mazuri kwa walimu na wanafunzi.

Mwenyekiti wa Chama cha Wamiliki wa Shule na Vyuo Binafsi Tanzania (TAMONGSCO), Mahmoud Mringo, alisema Serikali isidhani ni nafasi 10,000 zilizokosa wanafunzi, bali ni zaidi ya nafasi 30,000.

“Tumejiandaa vizuri kuwapokea wanafunzi wa kidato cha 5, si wale waliofeli tu, hata waliofaulu kwa kuwa kinachoangaliwa ni ubora wa elimu.

“Mfano ni sifa za kujiunga kidato cha 5, zimefanywa kubwa, hakuna sababu mwanafunzi aliyepata alama tatu za B akose nafasi ya kuendelea, hao sisi tutawapokea.

“Sekta binafsi tuna nafasi 36,000 ambazo zinahitaji wateja, tutawapokea tu, lipo tatizo kwa wanafunzi wetu, wanataka kwenda vyuoni zaidi kutafuta vyeti kuliko kuendelea kidato cha tano,” alisema Mringo.

CWT

Naye Katibu Mkuu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), Ezekiel Oluoch, alisema nafasi hizo ni upotevu mkubwa wa rasilimali watu.

“Kuna haja ya kuangalia kwa kina, tusiharibu kuanzia ngazi ya chini, maana vyuo vikuu vitaendelea kukosa wanafunzi kwa miaka ijayo,” alisema Oluoch.

Aliishauri Serikali kuwekeza zaidi katika sekta ya elimu kwa kuongeza bajeti, ili shule ziweze kuboresha vitendea kazi.

“Motisha kwa walimu, hasa wa Sayansi ni muhimu, takwimu zinaonyesha kuna upungufu mkubwa wa walimu si chini ya 20,000 katika shule za serikali.”

Alisema wanafunzi 5,000 wanaohitimu vyuo vya ualimu nchini wengi wao hawafanyi kazi ya ualimu, kutokana na mazingira mabovu yaliyopo ambayo yanachangia kushuka kwa kiwango cha elimu.

Alisema kulingana na hali ilivyo hivi sasa, kuna uwezekano mkubwa mwakani nafasi hizo kuongezeka kutoka 10,000 hadi 20,000.

MBUNGE KESSY

Mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki, Nderakindo Kessy, alisema changamoto inayoikabili sekta ya elimu inatokana na uongozi katika sekta hiyo kutobadilika kimtazamo.

“Kila kitu humu duniani kinabadilika, watoto wa leo wafikiria yao, tofauti na watoto wa zamani, tatizo je, viongozi wetu wanalijua hilo?

“Ufundishaji, utungaji mitihani na usahihishaji lazima uzingatie binadamu wa sasa alivyo, tatizo si kwa wanafunzi, bali ni uongozi usiotambua mabadiliko ya jana na leo,” alisema Kessy.

Aliongeza kuwa uongozi unaoendana na itikadi za kisiasa ndiyo chanzo cha mdororo wa elimu nchini.

Februari mwaka huu, uliibuka mjadala mzito baada ya Serikali kutangaza matokeo ya kidato cha nne, ambapo asilimia 60 ya wanafunzi walidaiwa kufeli.
MTANZANIA
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...