Blogger Widgets

Social Icons

Pages

Wednesday, July 17, 2013

DAWA ZA KULEVYA NI VITA YA WOTE SIYO POLISI PEKE YAO

Waziri Mkuu Mizengo Pinda.
TAARIFA ya kukamatwa kwa wasichana wawili nchini Afrika Kusini wakiwa na shehena kubwa ya dawa za kulevya inazidi kusikitisha na kuhuzunisha sana!
Madawa ya kulevya.
Dawa za kulevya ni janga la taifa katika nchi yetu na sijaona mikakati yoyote ikifanywa na vyombo vya dola kwa kushirikiana na wananchi wema kuhakikisha tatizo hili linakuwa historia nchini mwetu.
Wakati umefika wa kila Mtanzania kutambua ubaya wa dawa hizi katika jamii na wahusika kama vile polisi, mahakimu, majaji, waendesha mashitaka na wananchi kuhakikisha wanaohusika na uingizaji, usambazaji na utengenezaji kama wapo nchini, wanafichuliwa na kufikishwa katika vyombo vya sheria.

Kila idara kati ya hizo nilizozitaja, ikilegea inakuwa kama wametoa mwanya kwa dawa hizo kutapakaa nchini na kuathiri watumiaji.
 Nakumbuka maadhimisho ya kitaifa ya ‘Siku ya Kupiga Vita Dawa za Kulevya Duniani’ yaliyofanyika mwezi uliopita, Waziri Mkuu Mizengo Pinda alitangaza kwamba tatizo la dawa hizo ni janga la kitaifa hivi sasa.
Akasema kumekuwa na wimbi kubwa la Watanzania wanaojiingiza katika biashara hiyo haramu ya dawa za kulevya ndani na nje ya nchi na kwamba, katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, watuhumiwa 10,799 walikamatwa kwa kujihusisha na dawa hizo.
Pia alisema katika kipindi hicho, Watanzania 240 walikamatwa katika nchi za Brazil, Pakistan na Afrika Kusini, kuharibu taswira ya nchi na kusababisha Watanzania wasio na hatia kupata usumbufu na masharti magumu wanapotaka kusafiri kwenda nchi mbalimbali duniani.
Anasema mwaka huu pekee kumekuwa na ukamataji mkubwa wa dawa za kulevya katika eneo la kimataifa la Bahari ya Hindi karibu na nchini .
Ni wazi kuwa kauli hiyo ya Pinda inathibitisha dhahiri kuwa taifa linakabiliwa na changamoto kubwa ya kudhibiti tatizo la dawa za kulevya.
Ninachosema ni kwamba vita bado ni ngumu kutokana na wanaoendesha biashara ya dawa hizo kuwa na fedha za kutoa rushwa kwa lengo la kuzuia kukamatwa.
Kutokana na hali hiyo, hivi sasa biashara hiyo inaendelea kusambaa na kwamba, tayari imeshabisha hodi hadi shuleni, kwa wasanii, wanamuziki na hata kwa wachezaji wa michezo mbalimbali.
Nilishituka Waziri Mkuu Pinda aliposema kuwa  hivi sasa mikate, maandazi na askrimu zinazouzwa kwenye shule za msingi, zinawekwa dawa za kulevya.
Akabainisha kuwa vitendo hivyo vinafanya vijana wengi wa shule za msingi na hata sekondari kuwa na tabia za ajabu, ikiwamo kuingia darasani wakiwa na kiatu kimoja mguuni, mkufu wenye nyembe na kidani chenye nyembe kifuani.
Natoa wito kwa kusema vita dhidi ya matumizi na biashara haramu ya dawa za kulevya inahitaji ushirikiano wa hali ya juu kwa Watanzania wote bila kujali itikadi.
Polisi wafanye kazi yao, mahakama nayo ifanye kazi yake sawasawa kwani kuna taarifa kuwa kesi za dawa za kulevya nchini ni chache sana zinazoisha; Nyingi zipo mahakanani, zinakwamishwa na nini?
Dunia nzima inapiga marufuku dawa za kulevya kwa sababu huchangia makosa mengi kutendwa kama vile wizi, uporaji, ukabaji na hata ujambazi na watumiaji kuharibikiwa akili, hivyo kupoteza nguvu kazi ya taifa.
Kwa hiyo vita dhidi yake ni wajibu wa kila mtu.
Cha kusikitisha na kuhuzunisha ni kwamba, mara zote vinapotajwa vikwazo vinavyokwamisha vita dhidi ya dawa za kulevya, kiini hasa cha tatizo huwa hakiguswi kabisa!
Kiini hicho si kingine, bali ni unafiki, wanakamatwa watu wadogowadogo sana na mapapa hawapo, asili ya matumizi ya dawa za kulevya haisemwi! Kwamba ni unywaji wa pombe.
Kabla ya dawa za kulevya hazijagunduliwa, wanywaji walikuwa wakinywa pombe ya kawaida.
Pombe ya kawaida ilipoonekana inachelewesha lengo la mnywaji, ikatengenezwa gongo, na kadhalika. Pombe kali ilipoonekana inachelewesha lengo, ndiyo sasa zikavumbuliwa dawa za kulevya. Lengo likiwa lilelile, kuharakisha kulewa. Huo ndiyo ukweli, ambao watu hawataki kuusema.
Baadaye watu wakaunda usemi kuhalalisha ulevi eti kuna kuna pombe haramu na pombe halali!
Tujiulize,  lengo la mnywaji wa gongo lina tofauti gani na lile la mnywaji wa wiski? Tunajua kuwa pamoja na manufaa ya kiuchumi yaliyomo kwenye biashara ya pombe, madhara yake (pombe) ni makubwa sana kwa jamii na moja ni hili la vijana kutumia dawa za kulevya. Kwa kuwa kuna ugumu wa kuzuia na kupiga vita unywaji wa pombe, vita dhidi ya dawa za kulevya kamwe haitafanikiwa.
Haitafanikiwa pia kama wenye mamlaka au jamaa zao wataendelea kuwa sehemu ya dawa za kulevya, pia ikiwa vyombo vinavyohusika na mapambano vitakabiliwa na tatizo la rushwa.
Wito ninaoutoa ni kwamba, kesi zilizopo mahakamani zishughulikiwe na ikiwezekana Rais Jakaya Kikwete aunde mahakama maalum ya kushughulikia watuhumiwa wa dawa za kulevya ili kesi zisiwe zinachewa sana kama ilivyo sasa.

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...