Blogger Widgets

Social Icons

Pages

Wednesday, July 31, 2013

Wasomali washtushwa na mashambulizi ya al-Shabaab dhidi ya 'ndugu wa Kiislamu' wa Kituruki

Vikosi vya usalama vya Kituruki na Kisomali nje ya jengo la ubalozi wa Uturuki baada ya mshambuliaji wa kujitoa mhanga kulilipua lango la jengo hilo. [Majid Ahmed/Sabahi]
l-Shabaab inatekeleza ahadi yake ya kuendeleza ghasia wakati wa Ramadhani huku mashambulizi ya mwisho kabisa yakiwa ni kwenye Ubalozi wa Uturuki mjini Mogadishu mwishoni mwa wiki.
Mara moja viongozi wa Somalia na Uturuki waliyalaani mashambulizi hayo, na kuapa kwamba yasingeliitikisa nia yao ya kupambana na ugaidi na kujenga ushirikiano ambao nchi hizo mbili zimeuunda kwa miaka michache iliyopita.
Kiasi cha watu sita waliuawa kwenye mashambulizi hayo, ikiwa ni pamoja na mlinzi wa Kituruki, raia wawili wa Kisomali na wanamgambo watatu wa al-Shabaab, mfanyakazi wa ubalozi huo Abdi Mohamed aliiambia Sabahi. Watu tisa walijeruhiwa, wakiwemo maafisa wanne wa kikosi cha usalama cha Uturuki waliokuwa kwenye zamu ya kulinda jengo hilo.

Mashambulizi hayo yalianza pale mlipuaji wa kujitoa mhanga wa al-Shabaab alipolilipua gari lenye mabomu kwenye lango la kuingilia jengo hilo. Kisha wapiganaji wawili wenye silaha wa al-Shabaab walijaribu kuingia kwenye jengo hilo lakini walikabiliwa na vikosi vya usalama vya Uturuki na kuuawa kabla ya kulifikia jengo, kwa mujibu wa wafanyakazi wa Kisomali wanaofanya kazi kwenye ubalozi wa Uturuki ambao walizungumza na Sabahi.

Mtu aliyejeruhiwa vibaya akiwekwa ndani ya gari ya wagonjwa muda mfupi baada ya mashambulizi ya bomu. [Majid Ahmed/Sabahi]

Katika jaribio la kuhalalisha mashambulizi hayo, al-Shabaab ilituma ujumbe kwenye Twitter ikiitaja Uturuki "nchi isiyo ya Kiislamu".

"Waturuki ni sehemu ya kundi la mataifa yanayoiunga mkono serikali ya kikafiri na yanayojaribu kukandamiza uanzishwaji wa mfumo wa Sharia ya Kiislamu," ulisema ujumbe huo.


Msemaji wa al-Shabaab, Ali Mohamud Rage, aliapa kwamba kundi hilo la wanamgambo litaendelea kuwalenga raia wa Uturuki nchini Somalia.

"Mujahidina wataendeleza mashambulizi yao yanayowalenga maafisa wa serikali ya Uturuki mjini Mogadishu hadi Uturuki itakapoacha kuingilia mambo ya ndani ya Somalia," alisema Rage kwenye taarifa iliyotangazwa na Redio Andalus, inayotumiwa na kundi hilo.

Rage aliwaelezea wafanyakazi wa huduma za dharura na wanadiplomasia wa Kituruki nchini Somalia kama makafiri "ambao kwa hakika wamewasababishia Waislamu, hasa nchini Somalia, matatizo mengi na kupanga njama dhidi yao."

"Inawezekana kuwa watu wengi watajiuliza kwa nini watu wa Uturuki, ambao ni Waislamu, walishambuliwa, lakini tunataka kuwawekea watu wazi kwamba Uturuki imeutelekeza Uislamu na dini ya Mungu," alisema. "Wameishambulia nyumba ya Waislamu."

Uvamizi usio wa haki
Shambulio hilo lilisababisha malalamiko kutoka sehemu kubwa ya viongozi wa Somalia, Uturuki na wa kimataifa, pamoja na kutoka kwa raia wa Somalia.

"Shambullio hilo dhidi ya waajiriwa wa Uturuki ambao walikuja Somalia kusaidia Wasomali haliwezi kuhalalishwa hata kidogo," alisema Mohamed Osman, ofisa mstaafu kutoka Shirika la Upelelezi na Usalama la Taifa.

"Waajiriwa wa Uturuki ambao walikuwa walengwa katika shambulio hili la kutisha siyo tu askari lakini raia ambao wanafanya shaghuli za kihalali za kibinadamu katika nchi yetu," Osman aliiambia Sabahi. "Wamekuwa wakifanya kazi usiku na mchana kusaidia watu wa Somalia na kwa hiyo kitendo hiki cha kutisha sana hakiwezi kuhalalishwa kwa namna yoyote ile."

"Wasomali wote wanalaani kitendo hiki kibaya, ambacho kinaonyesha makusudio mabaya ya magaidi," alisema. "Shambulio hili dhidi ya waajiriwa wa Uturuki huko Mogadishu linawakilisha shambulio dhidi ya watu wa Somalia."

Rais wa Somalia Hassan Sheikh Mohamud alielezea shambulio hili kama "kiitendo cha uoga wa kukata tamaa na magaidi ambao hawajali lolote kwa ajili ya amani au utulivu wa Somalia", alisema wakati akitoa rambirambi zake kwa watu na serikali ya Uturuki.

"Ninalaani kitendo hiki cha jinai cha ugaidi na serikali yangu na vikosi vya usalama vitafanya kila kinachowezekana kuwakamata waliopanga na kuielekeza," Mohamud alisema katika taarifa mara tu baada ya shambulio.

"Lazima tuendelee kusimama imara dhidi ya wale wanaotafuta kuharibu nchi hii na, kwa msaada wa kijasiri wa washirika wetu, lazima tuongeze jitihada zetu mara mbili ili kutoa siku zijazo za amani kwa watu wa Somalia ambao wanahitaji sana," alisema.

Mohamud aliusifu msaada wa Uturuki kwa Somalia, akiitaja serikali ya Uturuki moja kati ya "mshirika anayetumainiwa na kutegemewa wa Somalia".

Uturuki ilianzisha kampeni kubwa ya kidiplomasia na kibinadamu miaka miwili iliyopita na imetoa mchango mkubwa katika jitihada za ujenzi mpya katika Somalia.

Shirika la ndege la Uturuki lilikuwa shirika la kwanza la kimataifa katika miongo miwili kufanya safari za mara kwa mara kwenda Mogadishu na kuna mamia ya wafanyakazi wa misaada wa Uturuki huko Mogadishu.

"Waturuki wengi wamekuja Somalia kusaidia kujenga tena kwetu," Mohamud alisema. "Tuna shule mpya na hospitali kwa sababu ya kazi yao ya kipekee."

Hitilafu ya Al-Shabaab
"Kitendo hiki kinathibitisha tena kinyume cha kile vikundi vya wanamgambo magaidi vinachodai vinapigania," alisema Omar Foodaadi,mwenye miaka 49, mchambuzi wa mambo ya siasa huko Mogadishu.

"Al-Shabaab ingewaeleza wafuasi wake kwamba inaendesha vita vitakatifu dhidi ya makafiri lakini ukweli ilikuwa inawalenga Waislamu wasio na hatia wakati wa mwezi mtukufu wa Ramadhani kwa kuwa ilionyesha wazi, kwa mara nyingine, inapuuza maisha ya binadamu kwa kuwalenga raia wasio na hatia kutoka katika nchi ya Waislamu," alisema.

"Magaidi wakati wote wanajaribu kuzuia maendeleo ambayo Somalia inayapata kwa sababu hawataki kuanzishwa kwa taifa la Somalia," Foodaadi aliiambia Sabahi. "Ni watu wanaofaidika na vurugu lakini vurugu hazidumu milele."

Watu huko Mogadishu walionyesha wasiwasi wao kuhusu vitisho na mashambulio ya mauaji yasiyobagua ya al-Shabaab yanayowaumiza wananchi.

"Nilishtushwa sana niliposikia habari kuhusu shambulio la mauaji na vitisho ambavyo al-Shabaab wanafanya dhidi ya mashirika ya kutoa misaada ya Uturuki ambayo yamekuwa yakitusaidia," Adam Bile, baba wa watoto wanne mwenye umri wa miaka 56 ambaye anaishi katika kambi kwa ajili ya watu wasiokuwa na makazi za Tarabuunka huko Mogadishu, aliiambia Sabahi. "Hawa ni ndugu zetu wa Kiislamu na ninaona hili kama jeraha kwa mahitaji yetu ya msaada kutoka kwa Waislamu."

Amina Hirsi, mama wa watoto saba mwenye umri wa miaka 41 anayeishi katika kambi ya Badbado huko Mogadishu, alihoji azma ya al-Shabaab kulenga wafanyakazi wa kutoa misaada wa Kituruki na wanadiplomasia.

"Nimechanganyikiwa kuhusu kama viongozi wa al-Shabaab wamepoteza mwelekeo walipoondolewa Mogadishu na kuona mabadiliko ya usalama na kurejea kwa upatikanaji wa misaada kwa watu, au kama hawawezi kuelewa maana ya malengo ya kidini wanayodai kuyapigania," aliiambia Sabahi.

"Samahani kwamba magaidi wa al-Shabaab waliwashambulia ndugu zetu Waturuki," alisema.

"Lolote lililotokea, ninaamini tulihisi maumivu yale yale kama ndugu zetu wa Uturuki walivyohisi," alisema Habiba Dahir, mama wa watoto watatu mwenye umri wa miaka 35 ambaye anaishi katia kambi ya Badbado.

"Nilitambua wakati al-Shabaab waliposhambulia ndugu zetu wa Kiislamu kwamba inathibitisha jinsi al-Shabaab wanavyotaka kuumiza na kumdhuru Muislamu yeyote anayetaka kutusaidia," aliiambia Sabahi. "Wamepoteza mwelekeo wa jihad ambayo Mungu alifafanua kwetu katika dini. Ningesema kwa mataifa ya Kiislamu, yasisimame na kuangalia tu matatizo ambayo al-Shabaab wanatuumiza nayo, lakini yajaribu kutusaidia."

Mshikamano ni imara baina ya Somalia, Uturuki
Waziri Mkuu wa Somalia Abdi Farah Shirdon, Waziri wa Mambo ya Ndani Abdikarin Hussein Gulled, Waziri wa Ulinzi Abdihakin Haji Mohamud Fiqi, Waziri wa Fedha Mohamud Awil Suleiman na maafisa wengine wa serikali ya Somalia walitembelea eneo la mlipuko siku ya Jumapili ili kuonesha mshikamano wao na Uturuki na kulaani shambulio hilo la kujitoa mhanga.

"Tendo kama hilo la kigaidi lililoshindwa halitaathiri uhusiano baina ya Somalia na Uturuki na halitarejesha nyuma njia ya mafanikio, ambayo yamekuwa yakipatikana Somalia yote," Shirdon alisema katika mkutano wa pamoja kwa waandishi wa habari pamoja na Balozi wa Uturuki Somalia Kani Torun.

Shirdon pia alitilia mkazo mshikamano wa watu wa Somalia na serikali yake kwa familia za wahanga wa Kituruki waliopoteza wapendwa wao kutokana na shambulio hili.

"Katu hatutasimamisha juhudi zetu bila ya kuchoka za kuwasaidia watu wa Somalia ili warejee hali zao baada ya miaka ya misukosuko na miradi inayoendelea ya maendeleo inayofadhiliwa na Uturuki itamalizwa," Torun alisema.

Mkurugenzi Mkuu katika Wizara ya Mambo ya Ndani na Usalama wa Taifa Hussein Abdi Aden alisema serikali imedhamiria kulinda misheni za kigeni zilizoko Somalia.

"Kuwalenga waajiriwa wa kiraia kunaonesha ukosefu wa heshima kwa upande wa magaidi kwa maisha ya binadamu na wanadiplomasia wa kigeni ambao wamekuja Somalia kuwasaidia watu wetu," aliiambia Sabahi.

"Tendo hili la kigaidi lina sifa ya kiwango kikubwa cha uoga," alisema. "Magaidi wanawalenga wafanyakazi wa kiraia wa Uturuki kwa sababu ya jukumu la Uturuki katika kuwasaidia watu wa Somalia."


Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...