Blogger Widgets

Social Icons

Pages

Saturday, May 25, 2013

WAKALA NA MAMLAKA ZA SERIKALI ZIMEHIMIZWA KUWEKA MIKAKATI YA KUJIENDESHA KWA FAIDA BILA KUITEGEMEA SERIKALI

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

OFISI YA RAIS

TUME YA UTUMISHI WA UMMA

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

WAKALA NA MAMLAKA ZA SERIKALI ZIMEHIMIZWA KUWEKA MIKAKATI YA KUJIENDESHA KWA FAIDA BILA KUITEGEMEA SERIKALI   

Wakala na Mamlaka za Serikali wamehizwa kuweka mikakati ya kujiendesha kwa faida, kuwa wabunifu, wakabiliane na changamoto zilizopo na pia watekeleze majukumu yao kwa kufuata Sheria, Kanuni na Taratibu zilizowekwa bila kutegemea fedha kutoka Serikalini. Wametakiwa katika mipango na malengo yao, vipaumbele vyao viwe ni rasilimali watu, matumizi bora ya rasilimali fedha na utoaji wa huduma bora kwa wananchi. Kwa kufanya hivyo, adhma ya Serikali ya kuzifanya Wakala na Mamlaka zijitegemee zenyewe itaweza kufikiwa endapo wataongeza uzalishaji na hatimaye mchango wao kwa Taifa utaonekana kupitia maendeleo yatakayopatikana.
Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Umma katika Ofisi ya Rais, Bwana Jovin Kitambi kwa nyakati tofauti jijini Dar es Salaam  wakati akizungumza na Menejimenti na Watumishi wa Wakala wa Huduma ya Umeme, Mitambo na Huduma za Elekronikia Tanzania (TEMESA), Mamlaka ya Usafiri na Usalama wa Anga Tanzania (TCAA) na Wakala wa Vyuo vya Mafunzo ya Mifugo Tanzania (LITA).
“Miongoni mwa sababu zilizosababisha Mashirika mengi yaliyokuwa yanamilikiwa na Serikali kufa ni kutokana na kuwepo kwa Menejimenti mbovu zilizokuwa zimepewa dhamana ya kusimamia mashirika hayo. Hivyo, Serikali iliamua kuunda Wakala na Mamlaka mbalimbali kwa lengo la kuona zinajiendesha kwa faida, kwa ufanisi na zinatoa huduma bora. Serikali haitakuwa tayari kuona Wakala na Mamlaka zilizoanzishwa zinakufa kutokana na Menejimenti mbovu” amesema Kitambi.

Kitambi amesema “hivi sasa kumekuwa na ubadhilifu baadhi yenu mnakusanya mapato mnayachezeachezea kwa kuwa na matumizi mabovu. Simamieni rasilimali watu, nidhamu na uadilifu katika utekelezaji wa majukumu yenu ili muweze kuisaidia Serikali na lengo la nyinyi kuwa Wakala na Mamlaka liweze kuwa na tija. Ni lazima  mjiendeshe kwa faida, ufanisi na mnakuwa wabunifu ili kukabiliana na changamoto mbalimbali zilizopo na hatimaye muweze kutoa mchango wenu kwa kuleta maendeleo ya nchi hasa pale mtakapoweza kukusanya mapato na kuyaelekeza katika matumizi ya maendeleo”.
“Wakala na Mamlaka za Serikali ni Watumishi wa umma hapa nchini, miongoni mwenu mnalalamikiwa sana na wananchi kwa jinsi mnavyotoa huduma zenu na  maadili ya kazi yamekuwa hayasimamiwi vizuri. Hivyo ni lazima mbadilike, msifanye kazi kwa mazoea, hakikisheni mnaendesha shughuli zenu mkiwa watumishi wa umma kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Taratibu zilizopo. Kwa kufanya hivyo, mtakuwa mnatimiza wajibu wenu ipasavyo na mnaisaidia Serikali. Pia mtakuwa mmeondoa malalamiko mengi ya wananchi kuhusu utendaji kazi wa watumishi wa umma” amesisitiza bwana Kitambi.
“Ni aibu sana kwa mtumishi wa umma kupatikana na makosa ya uvunjaji wa Sheria anapotekeleza majukumu yake kwa kwenda kinyume na maadili ya msingi. Kuna baadhi ya watumishi wamechukuliwa hatua za kinidhamu kwa kutenda makosa mbalimbali mfano kudai na kuopokea rushwa, ubadhirifu, wizi wa mali ya umma, utoro kazini, ubakaji, kudanganya na kuajiliwa kinyume na sifa na hali hii inaitia doa kubwa Serikali” amesema.
Kitambi amesema Tume za Utumishi wa Umma zipo karibu nchi zote duniani na zimeanzishwa kwa lengo la kusimamia uendeshaji wa rasilimali watu katika utumishi wa umma na kuhakikisha unaleta tija. Amewataka Waajiri,Mamlaka za Ajira na Nidhamu kuzisimamia Sheria, Maadili na Nidhamu.
“Waajiri na Watendaji Wakuu mnapaswa mfahamu kuwa rasilimali watu ni muhimu sana katika maendeleo ya Wakala na Mamlaka zenu. Utumishi wa umma hauongozwi hivi hivi tu, unaongozwa kwa mujibu wa Sheria, Kanuni na Taratibu, na tunapozikiuka tunazua malalamiko mengi kwa wananchi. Wasimamieni watumishi walio chini yenu ipasavyo kwa kuhakikisha kila mtumishi wa Wakala na Mamlaka anapangiwa majukumu ya kufanya kulingana na taaluma yake, kunakuwepo na ufuatiliaji, simamieni maadili bila kuona aibu wala upendeleo, fanyeni kazi kwa misingi iliyowekwa na mkimtendea haki kila mtumishi. Maana siku hizi kuna malalamiko pia yanatolewa na watumishi ndani ya Wakala na Mamlaka pale yanapofanywa mambo kienyeji enyeji tu, matokeo yake ni kupunguza ari kwa watumishi ya kufanya kazi” amesema.
“Waajiri na Uongozi mzima wa Menejimenti ni lazima maslahi ya watumishi wenu ikiwemo mishahara yapewe kipaumbele, muwe na mpango wa mafunzo ili watumishi walio chini yenu waweze kujiendeleza, wapandisheni vyeo watumishi bila upendeleo, itisheni vikao na watumishi wenu, toeni maamuzi sahihi kwa wakati, na pia muajiri watumishi  kwa kuzingatia taaluma na sifa. Bila kuyasimamia haya na endapo ikithibitika, Serikali haitasita kumchukulia hatua Mwajiri au Mtendaji Mkuu yeyote ambae atakwenda kinyume kwa kutokusimamia Sheria na kutenda haki ipasavyo” amesisitiza.
Akizungumzia upande wa waajiri kutokujibu na kutoa ufafanuzi wa kero za wananchi amesema wananchi wanalalamika wamekuwa wakiandika barua kwa Wakala na Mamlaka mbalimbali kuhusiana na kero zao lakini wamekuwa hawajibiwi kwa waajiri kuona kujibu barua si jambo la msingi, amewataka waajiri kujibu barua kwa wananchi kwa kuzingatia muda waliojiwekea katika mikataba yao ya huduma kwa wananchi.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Mamlaka ya Usafiri na Usalama wa Anga Tanzania (TCAA), Bwana Leuben Ruhongole kwa niaba ya Mtendaji Mkuu amesema, kwa kipindi chote tangu wakiwa Idara ya Usalama na Usafiri wa Anga baada ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kuvunjika mwaka 1977, wamepiga hatua kubwa, mwaka 1999 Serikali iliunda Wakala wa Usalama wa Anga na kutokana na kuendesha Wakala hiyo kwa faida kupitia Sheria Namba 10 ya mwaka 2003 pamoja na marekebisho yake ya mwaka 2006 imeweza kuwa Mamlaka kamili kuanzia mwaka 2003.
“Tumefanikiwa kwa kiasi kikubwa kuiendesha Mamlaka yetu kwa faida na ufanisi mkubwa kutokana na sisi wenyewe kusimamia majukumu yetu kikamilifu, kwa kufanya hivyo tumekuwa na makusanyo ya mapato yanayotuwezesha kujiendesha kupitia tozo mbalimbali tunazotoza ikiwa ni pamoja na kuongoza na kutoa taarifa za ndege, na pia tunalipwa na ndege husika pale inapokatiza anga la Tanzania. Tumefanikiwa kujenga jengo la Ofisi yetu linaloitwa Aviation House lililopo Ukonga Banana kutokana na mapato yetu.  Changamoto kubwa tuliyo nayo sisi kama Mamlaka ni ununuzi wa rada nyingine mpya ya kuongoza ndege ambayo ni gharama kubwa, kwa sasa rada iliyopo muda wake umekaribia kumalizika, ambao kwa kawaida muda wa rada kutumika ni miaka kumi” amesema.

Imetolewa na:
KITENGO CHA MAWASILIANO SERIKALINI
OFISI YA RAIS, TUME YA UTUMISHI WA UMMA
DAR ES SALAAM

25/05/2013
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...