Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete
amewashangaa baadhi ya wanasiasa ambao amewaeleza kuwa hawana shukurani
vinywani mwao na wala hawana macho ya kuona mafanikio ya dhahiri ya
Serikali katika sekta mbali mbali ikiwemo ile ya barabara na ujenzi wake
nchini.
Zaidi,
Rais Kikwete amewashangaa baadhi ya wanasiasa wa Mikoa ya Kusini ambao
wamekuwa wanalalamikia kutokumalizia kwa kipande kifupi cha barabara la
Somanga-Nyamwage kuwa ni kushindwa kutimizwa kwa ahadi za Rais Kikwete.
Akizungumza
juzi, Jumamosi, Aprili 13, 2013 katika Kijiji cha Kasera, Wilaya ya
Mkinga, Mkoa wa Tanga wakati wa uzinduzi wa Barabara ya lami ya
Tanga-Horohoro yenye kilomita 65.14, Rais Kikwete alisema:
“Hakuna
mtu yoyote ambaye haoni kuwa barabara hii ni ukombozi mkubwa wa
wananchi ambao huko nyuma hawakuwa na barabara ya lami, isipokuwa wale
wenye macho lakini wanajifanya hawaoni. Hawa ni watu wenye hiana mioyoni
mwao na hata Serikali ifanye nini wataendelea kuimba santuri yao ambayo
sasa imewachosha watu.”
Aliongeza
Rais Kikwete: “Wapo watu wanaoendelea kudai kuwa hakuna kilichofanyika.
Hawa ni sawa na wale watu wawili ambao walikuwa wanapoteza muda wake
kubishana mchana kweupe kuhusu kile walichokuwa wanakiona juu yao kama
ni Jua ama Mwezi. Ni wapuuzi tu.”
Kuhusu
malalamiko ya baadhi ya wabunge wa Mikoa ya Kusini juu ya Barabara ya
Lindi-Kibiti na hasa sehemu ya Nyamwage-Somanga, Rais Kikwete alisema:
“Hawa
ni watu ambao hawana hata shukurani vinywani mwao. Hapa ni mahali
hapakuwa na barabara kabisa wala Daraja lile la Mkapa. Wakati Mzee Mkapa
alipojenga Daraja la Mkapa wakamkejeli kuwa alichokuwa amefanya ni sawa
na kumnunulia shati mzazi wake aliye uchi. Atatoka vipi nje na shati
tupu?”
“Tulichofanya
sisi ni kujenga barabara yote hii ya lami kutoka Lindi hadi Kibiti. Hii
ilikuwa ni barabara iliyokuwa haipitiki wakati wa majira fulani fulani.
Tumemaliza kuijenga yote isipokuwa kilomita 9.5 ambazo nazo
wanamalizia. Sasa watu hawa, wanasiasa hawa wanataka tuwafanyie nini?
Barabara haikuwepo kabisa na zimebakia kilomita 9.5 tu na bado
wanalalamika na kusema Serikali gani hii? Wanataka tufanye nini?”
Wiki
iliyopita Bungeni Dodoma Mbunge mmoja wa Viti Maalum wa Chama cha CUF
alidai kuwa ahadi ya Mheshimiwa Rais Kikwete kujenga Barabara ya lami ya
Lindi-Kibiti ilikuwa haitekelezwi kwa sababu ya kutokamilika kwa sehemu
ya Somanga-Nyamwege. Mbunge huyo aliungwa mkono na wabunge kadhaa
kutoka Mikoa ya Kusini.
Rais
Kikwete pia amekumbushia kuwa katika miaka saba tu, Serikali yake
imekomesha aibu ya watu wanaokwenda sehemu moja ya nchi kulazimika
kupitia nchi jirani ili wafike.
“Tumesahau
kuwa miaka michache tu iliyopita watu wa kwenda Mwanza na Musoma
walikuwa wanapitia Nairobi na Kisumu katika Kenya? Watu wa kwenda Bukoba
walikuwa wanapitia Nairobi, Kampala, Masaka ndiyo wafike Mutukula
kuingia Tanzania? Tumesahau haya katika muda mfupi tu wa miaka saba?”
Barabara
ya Tanga-Horohoro ni moja ya miradi mingi ya miundombinu ambayo
inajengwa chini ya ufadhili wa Mpango wa Millenium Challenge
Account (Tanzania) wa Shirika la Millenium Challenge Corporation (MCC)
wa Marekani.
Ujenzi wa
barabara hiyo umegharimu Sh. Bilioni 75.715 ambazo zilikuwa ni pamoja
na fidia kwa nyumba na mali nyingine za wananchi pamoja na ujenzi wa
misikiti mipya kuchukua nafasi ya misikiti iliyovunjwa kupisha barabara.
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu.
Dar es Salaam.