Mkemia
kutoka Vinasaba kutoka Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali(GCLA) Fidelis
Segumba(kulia) akiwaeleza waandishi wa habari juu ya matumizi ya
Teknolojia ya Vinasaba vya Binadamu leo Jijini Dar es Salaam kushoto ni
Mkuu wa kitengo cha Sayansi ya Makosa ya Jinai Biologia na Vinasaba
kutoka kutoka ofisi hiyo Bi. Gloria Machuve.
PICHA ZOTE NA FRANK MVUNGI
……………………………………………….
Na Fatma Salum – MAELEZO
Serikali kupitia ofisi ya Mkemia
Mkuu wa Serikali ina mpango wa kuanzisha utaratibu wa kutambua raia wake
kupitia taarifa za vipimo vya vinasaba vya binadamu maarufu kama DNA.
Akifafanua mpango huo katika
mkutano wa waandishi wa habari na Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali
uliofanyika leo jijini Dar es Salaam, Mkuu wa Kitengo cha Sayansi ya
Makosa ya Jinai Biolojia na Vinasaba Gloria Machuve amesema kupitia
mfumo wa taarifa za vinasaba utaiwezesha serikali kutambua raia wake na
wahamiaji wasio raia kutokana na taarifa zao kutokuwepo kwenye mfumo
huo.
Bi Machuve ameeleza kuwa mpango
huo ukikamilika watanzania wataweza kupimwa vinasaba vyao na taarifa zao
zitawekwa kwenye mfumo rasmi wa taarifa (Database) hivyo kurahisisha
shughuli za uhamiaji ikiwemo utoaji wa pasipoti na vitambulisho vya
uraia.
Aidha mfumo huo utarahisisha
utambuzi wa viungo vya miili ya watanzania wanaofariki kwenye majanga
kama moto na ajali za vyombo vya usafiri wakiwa nje ya nchi kwani
taarifa za vinasaba vyao zitakuwepo kwenye mfumo hivyo zitaoanishwa na
majibu ya vinasaba vya viungo hivyo na hatimaye serikali kupata miili ya
raia wake.
Pia Bi Machuve ameongeza kuwa
kupitia mfumo huo utoaji wa vyeti vya kuzaliwa utaambatana na taarifa
kamili za vinasaba vya wazazi hivyo kurahisisha watu kupata vyeti
vyenye majina ya wazazi wao halali.
Naye Mkemia kutoka Wakala wa
Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali Fidelis Segumba amesema kuwa mfumo
huo pia utasaidia kupunguza tatizo la kubadilishwa watoto hospitalini
kwani utawezesha kutambua mama halali wa mtoto aliyezaliwa.
Segumba amesema faida nyingine za
mfumo huo ni pamoja na utambuzi wa viungo vya watu wenye ulemavu ngozi ,
kuondoa tatizo la watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi na
kutambua wahalifu husika wa makosa ya ubakaji.
Ili kufanikisha mpango huo Segumba
amesema serikali inabidi kuongeza wataalamu na kuongeza fedha kwa ajili
ya kununulia mitambo mingi ya kufanyia kazi hiyo.