Blogger Widgets

Social Icons

Pages

Wednesday, July 3, 2013

Marekani haijasaini mkataba wa ICC, lakini…

 

  • Hata hivyo mwenyewe Obama ameeleza wazi kuwa, hawezi kuitembelea Kenya wakati viongozi wake wa juu – Rais Uhuru Kenyatta na Makamu wake William Ruto ni watuhumiwa wa Mahakama ya Kimataifa ya uhalifu wa kivita (ICC).
Wakati huu ninapoandika makala hii, tuko kwenye pilikapilika za kumpokea Rais wa Marekani, Barack Obama. Kwa kweli ziara ya rais huyu imebadilisha kabisa ratiba za wakazi wa Dar es salaam.
Hata hivyo, kwa wenzetu Kenya imekuwa bahati mbaya. Huku wakiwa wamenuna, wamebaki na maswali mengi. Kwa nini Obama ambaye ana asili ya nchi hiyo hakupanga kufika kwao? Tanzania kuna nini hadi marais watatu tangu wa Marekani – Bill Clinton, George Bush na Obama wameitembelea?
Kumbuka Wakenya hawa wamekuwa wakifanya sherehe kubwa kila mara Obama anapopata mafanikio kisiasa. Alipoukwaa urais kwa mara ya kwanza mwaka 2008, walisherehekea. Mara ya pili mwaka 2012 walisimamisha kabisa kazi ili kusherehekea awamu ya pili ya urais wa Obama.
Lakini sasa Obama anafanya ziara ya pili Afrika bila kuitembelea Kenya na huenda hii ikawa ziara yake ya mwisho Afrika hadi atakapomaliza urais wake, kwa hiyo Wakenya hawana bahati.
Hata hivyo mwenyewe Obama ameeleza wazi kuwa, hawezi kuitembelea Kenya wakati viongozi wake wa juu – Rais Uhuru Kenyatta na Makamu wake William Ruto ni watuhumiwa wa Mahakama ya Kimataifa ya uhalifu wa kivita (ICC).
Ishara ya kutowatambua viongozi hao ilionekana tangu waliposhinda uchaguzi mkuu mwaka huu ambapo taarifa ya Serikali ya Marekani iliishia tu kuwapongeza Wakenya kwa kufanya uchaguzi ulio huru na wa haki, lakini haikuwataja Kenyatta na Rutto ambao ndiyo washindi.
Si Marekani tu, hata Uingereza imekataa kuwatambua Kenyatta na Ruto kwa sababu hiyo. Mara baada ya ushindi wake, Kenyatta alizuru Marekani kwenye mkutano wa kutafuta suluhu ya Taifa la Somalia. Huko alikumbana na kituko baada ya Waziri Mkuu wa Uingereza, David Cameron kugoma kupiga naye picha.
Lakini swali moja linabaki, Marekani ina uhalali gani wa kuinyooshea kidole Kenya ikiwa yenyewe imegoma kusaini mkataba wa ICC (Rome Statute of the International Criminal Court)?
Hadi sasa kuna nchi 139 duniani zilizosaini mkataba huo. Nchi ambazo hazijasaini ikiwemo Marekani, haziguswi na hatia yoyote ya uhalifu wa kivita.
Marekani inajua wazi kwamba siku ikitia saini imeingia kwenye mtego wa kushtakiwa kutokana na makosa mengi ya uhalifu wa kivita iliyofanya.
Lakini leo Obama amesusa kwenda Kenya eti kwa sababu Kenyatta na Rutto ni washtakiwa wa ICC! Usishangae kusikia Marekani inayojiita kinara wa demokrasia duniani ikiwaunga mkono baadhi ya viongozi wa kiimla na wababe wa vita duniani.
Hiyo ndiyo Marekani inayoibembeleza Tanzania.

Chanzo: Mwananchi
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...