Blogger Widgets

Social Icons

Pages

Saturday, July 13, 2013

Mama ntilie jijini Dar watumika kuuza dawa za kulevya

Biashara ya dawa za kulevya nchini inazidi kuchukua sura mpya ambapo sasa wanawake wanaouza vyakula, maarufu mama ntilie, hutumika kusambaza dawa hizo kwa wateja. Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili kwa muda mrefu katika maeneo mbalimbali jijini Dar es Salaam unaonyesha kuwa biashara hiyo inafanyika katika maeneo ya Tandika, Manzese, Vingunguti, Temeke, Tandale, Mtongani na Keko.
Wanawake  hao wamekuwa wakitumia mwanya wa kuuza chakula kama kinga yao, huku biashara yao kubwa ikiwa ni kuuza dawa za kulevya aina ya heroin, bangi na aina nyingine.
 Mbinu hii mpya ya usambazaji wa dawa za kulevya kwa kutumia wanawake wanaouza vyakula imeelezwa kuwa inawasaidia wahusika wakuu, kuendesha biashara yao kwa ufanisi zaidi.
Uchunguzi umeonyesha kuwa wafanyabiashara wa dawa hizo wameamua kuwatumia mamalishe kutokana na kuwa waaminifu na kuhudumia wateja wengi, hivyo ni vigumu watu kuwashtukia wakiwamo askari polisi.
Imebainika kuwa dawa hizo huuzwa kulingana na maeneo, wakati maeneo ya watu wasiokuwa wa uwezo hupimwa kwa kutumia kipimo kidogo zaidi kwa bei ya chini ambayo watumiaji husika huweza kuimudu.
Aidha dawa hizo hufungwa katika mitindo miwili tofauti, ukiwa katika unga wa vidonge na wa kawaida ingawa bei zake hazitofautiani sana.
Uchunguzi unaonyesha kuwa vidoge huuzwa vikiwa vizima au vipande, huku unga wa kawaida ukiuzwa kwa kipimo maalumu.
Kwa kawaida ‘unga’ huo huuzwa kwa Sh1,000 kwa pointi huku kete moja ikiuzwa kwa Sh2,000, wakati vidonge, kizima huuzwa kwa Sh2,000, huku kipande huuzwa kwa Sh1,000 zikitofautiana kulingana na maeneo.
Gazeti hili lilifanikiwa kuongea na baadhi ya wanawake wanaojihusisha na uuzaji wa dawa hizo. 
Dada mmoja aliyejitambulisha kwa jina moja la Asha (28) ambaye siyo jina lake halisi ni muuzaji mkubwa wa dawa hizo. Awali alikuwa akifanya shughuli zake hizo za uuzaji katika maeneo ya Yombo Kilakala, ingawaje hivi sasa amehamia Temeke.
“Unajua siku zote dhumuni la kufanya biashara ni kupata faida, hivyo naweza kusema niliingia kwenye biashara hii kwa sababu tu ina faida zaidi kuliko biashara nyingine,” anasema.
Awali alikuwa akiuza vyakula huku akifanya biashara hiyo ya kuuza dawa, baadaye akaacha kuuza vyakula akabaki na biashara ya dawa za kulevya.
Akielezea namna anavyofanya biashara yake hiyo, Asha anasema kwa kawaida huwa ananunua mkanda ambao unakuwa umefungwa vidoge vidogovidogo kumi hadi ishirini. Mara nyingi huuza kulingana na mahitaji ya mteja.
“Halafu baada ya kununua hivyo huwa nauza kidogokidogo vidonge hivyo.
Kwa kawaida kidoge kimoja huwa nauza kati ya sh1,000 hadi Sh2,000.  Bei yake hutegemea na mahali unapouzia. Kama unauzia watu waliochoka sana inabidi upaki kidogokidogo ili kuweza kuliteka soko lao,” anasema.
“Nimefanya biashara hii kwa muda wa miaka mitatu, lakini ukweli ni kwamba hadi sasa nimefanikiwa kwa kiasi fulani. Nimeweza kujenga nyumba ya kwangu mwenyewe, pia kuhudumia familia yangu. Licha ya kuwa na madhara kwa watu, lakini ukweli ni kuwa biashara ya unga inalipa,” anasisitiza.
Abubakari Ismail (33) aliyewahi kutumia dawa za kulevya, ambaye kwa sasa ni kiongozi wa kupambana na dawa hizo kinachofahamika kama Use Ant -Drugs, kilichopo Yombo, wilayani Temeke, anasema kuwa tatizo la wanawake kujihusisha na uuzaji wa dawa za kulevya linachangia kwa kiasi kikubwa kuzorotesha mapambano dhidi ya dawa hizo hususan kwa vijana.
‘Joseph (17)’,  siyo jina lake halisi ni kijana aliyekuwa katika matibabu kutokana na matumizi ya dawa za kulevya. Hivi sasa kijana huyu amelazimika kuhama nyumbani kwao kutokana na kumkimbia mama yake mzazi ambaye anajihusisha na uuzaji wa dawa za kulevya.
Mkurugenzi wa Kituo cha Makangarawe Youth Information Center cha jijini Dar es Salaam, kinachojishughulisha na miradi kadhaa ya vijana ikiwamo mapambano dhidi ya dawa za kulevya kwa vijana, Ismail Mnikite, amesema kitendo cha wanawake kushiriki katika uuzaji wa dawa za kulevya ni tatizo jipya linalochangia kukwamisha juhudi za mapambano hayo.
Chanzo - Mwananchi
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...