Watoto saba ambao ni raia wa Burundi na Rwanda ambao walikamatwa wakati 
walipokuwa wakisafirishwa kutoka Burundi kuja Tabora kwa ajili ya kuuzwa
watumikishwe katika mashamba ya tumbaku,Watoto hawa walikamatwa eneo la 
Ulyankulu wilayani Kaliua wakiwa na tajiri yao ambaye amefahamika kwa 
jina la Emmanuel John(22) ambaye pia ni raia wa Burundi. 
Watoto wakiwa mahakama ya hakimu mkazi Tabora wakisubiri kuingia 
mahakamani kutoa ushahidi baada ya mtu aliyekuwa amewasafirisha kwa 
lengo la kutaka kuwauza kukamatwa na kufikishwa Mahakamani kujibu 
shitaka la kuwasafirisha kwa nia ya kuwafanyia biashara na kuingia 
nchini kinyume cha sheria.
Afisa na Mwanasheria wa Idara ya Uhamiaji mkoa wa Tabora akiwaongoza 
watoto hao kuingia chumba cha mahakama ya hakimu mkazi Tabora kwa ajili 
ya kutoa ushahidi dhidi ya Emmanuel John.
RAIA wa Burundi, Emmanuel John (22),aliyekamatwa akituhumiwa kusafirisha
 watoto,amefikishwa katika Mahakama ya Mkoa waTabora akikabiliwa na 
Mashitaka mawili moja likiwa ni la kuingia nchini kinyume cha sheria na 
kusafirisha binadamu kwa lengo la kutaka kuwauza.
Mbele ya Hakimu Mkazi Bw. Jackton Rushwela,Wakili wa Serikali Bw.Iddi 
Mgeni, alimsomea mshitakiwa mashitaka hayo ambapo alikiri kosa la 
kuingia nchini kinyume cha sheria huku kosa la pili la kuwasafirisha 
watoto hao saba akijaribu kutaka kuficha ukweli.
Kutokana na kukiri kosa la kwanza, Hakimu Rushwela alimhukumu kifungo cha mwaka mmoja jela au kulipa faini ya sh 100,000. 
Hata hivyo,mshitakiwa huyo Emmanuel John pamoja na kuiomba mahakama 
impatie fursa ya kumtaarifu mkewe aliyeko huko nyumbani kwao nchini 
Burundi kwa njia ya simu au apewe nafasi ya kuuza simu yake ya mkononi 
aweze kulipa faini hiyo kwa nia ya kutaka kujinasua na adhabu ya kifungo
 hicho cha mwaka mmoja lakini mahakama haikuwa tayari kutekeleza hilo.
Kuhusu shitaka la kusafirisha binadamu,upande wa mashitaka ulidai 
mshtakiwa alikamatwa na maofisa wa Idara ya Uhamiaji akiwasafirisha 
watoto Ndayisenga Batiliza(13), Ndakusenga Emmanuel(15), Nimbonajile 
Nagenda(13), Yazid John(15), James Justus(14) na Samson Banteke(17).
Baadhi ya watoto hao walitoa ushahidi walidai walisafirishwa na 
mshitakiwa Emmanuel John kutoka nchini Burundi na Rwanda hadi 
walipokamatwa eneo la Ulyankulu wilayani Kaliua.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi Julai 25, mwaka huu itakapoendelea tena kusikilizwa kwa mashahidi wengine kutoa ushahidi wao.






