- Ndiyo maana tunalalamikia sheria hiyo kwani kila wakati tembo wanauawa na hasa wale ambao wako nje ya hifadhi, kuna kigugumizi gani cha kutoleta sheria hiyo mapema bungeni.
 
Dodoma. Wizara ya Maliasili na Utalii inatarajia kuajiri askari 400 wa Wanyamapori nchini katika kipindi cha Julai mwaka huu.
Ahadi hiyo ilitolewa bungeni na Waziri wa 
Maliasili na Utalii Balozi Khamisi Kagasheki ambaye aliahidi pia 
kupeleka bungeni Sheria ya kuanzisha Mamlaka ya Wanyamapori katika Bunge
 la Novemba mwaka huu.
Alitoa kauli hiyo wakati akijibu swali la nyongeza
 la Zitto Kabwe (Kigoma Kaskazini-Chadema) ambaye alihoji mpango wa 
Serikali kuchelewesha kutungwa kwa mamlaka hiyo kuwa ni ukiukwaji na 
dharau kwa Bunge ambalo lilipendekeza hivyo.
“Ndiyo maana tunalalamikia sheria hiyo kwani kila 
wakati tembo wanauawa na hasa wale ambao wako nje ya hifadhi, kuna 
kigugumizi gani cha kutoleta sheria hiyo mapema bungeni,” alihoji Zitto.
John Lwanji (Manyoni Magharibi-CCM) alihoji mpango
 wa kuanzisha Mamlaka itakayosimamia hifadhi za mapori ya akiba ya 
wanyamapori badala ya idara ya wanyamapori.
Naibu Waziri wa Malisili na Utalii Lazaro Nyalandu
 alisema kuwa ahadi ya Serikali ya kuanzisha Mamlaka ya Wanyamapori iko 
palepale ambapo hadi sasa rasimu za kwanza za sheria hiyo 
zimekwishakamilika.
Nyalandu alisema kuwa katika mkutano wa nane wa 
Bunge, Serikali iliahidi kuwa ifikapo Desemba 2012, mchakato wa 
uanzishwaji wa Mamlaka ya Wanyamapori utakuwa umekamilika.
“Hata hivyo, baada ya kamati ya uanzishwaji wa 
Mamlaka kupata maoni ya wadau, iligundua uwepo wa mambo muhimu 
yaliyohitaji kujadiliwa kwa kina,” alisema Nyalandu.
Alizitaja sababu zilizochelewesha utaratibu huo ni
 kupanuka kwa wigo wa wadau kwani walikusanya maoni kutoka kwa watu 
wengi ambayo yanahitaji kufanyiwa kazi kikamilifu.
Chanzo: Mwananchi
Chanzo: Mwananchi



