Polisi Yawaonya Wanaokula Hadharani mwezi wa Ramadhani
POLISI Mkoa wa Kusini Pemba, limewataka wananchi kuwa na utamaduni
wa kuvumiliana kidini na kuheshimu imani za wengine, kwa kuepuka kula
hadharani katika mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhani kwani kufanya
hivyo kunaweza kusababisha uvunjifu wa amani miongoni mwa jamii.
Jeshi hilo limesema limejipanga kukabiliana na vitendo vyovyote vya
uvunjifu wa amani kama vile uvaaji wa mavazi yasioendana na maadili ya
kiislamu na kuhakikisha linakabiliana na uhalifu na wahalifu.
Kamanda wa Polisi wa mkoa huo, Saleh Mohammed Saleh, alitoa onyo hilo
wakati akizungumza na mwandishi wa habari hizo ofisini kwake Madungu
-Chake Chake Pemba.
“Tumejipanga vyema kufanya doria na oparesheni mbali mbali za kuwasaka
wahalifu wote ili kuona wananchi wa mkoa wa Kusini wanatekeleza ibada
yao kwa salama na amani,” alisema.
Aliwatanabahisha wananchi wote kuwa macho wakati wa kufutari kwani muda
kama huo ni mwanya kwa wahalifu kufanya makosa kwa kuvunja nyumba na
kuiba kwa vile wanajua watu wako katika harakati za futari.
Alisema katika kipindi cha Ramadhani, wahalifu hutumia mwanya huo
kufanya wizi wa mazao zikiwemo karafuu, ndizi, muhogo na nazi, hivyo ni
lazima wawe waangalifu na kudumisha ulinzi shirikishi katika maeneo yao.
Aidha amewataka madereva kutii sheria za barabarani, hususani nyakati za
kufutari kwa kuepuka kwenda mwendo wa kasi na kupakia abiria kupindukia
uwezo wa gari.
Zanzinews