Blogger Widgets

Social Icons

Pages

Thursday, July 18, 2013

Jengo Karibu na Ikulu noma ....... Vigogo wawili wa Wakala wa Majengo Kortini

Wakala wa Jengo lililojengwa mita chache kutoka Ikulu jijini Dar es Salaam.kulia ni Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), Mkaumba Kimweri (mbele)na Msanifu Mkuu, Richard Maliyaga, walipofikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam jana kujibu mashitaka matano ya matumizi mabaya ya madaraka.PICHA: OMAR FUNGO
 
*********
Mtemdaji Mkuu na Msanifu Mkuu wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam wakikabiliwa na mashitaka matano ya matumizi mabaya ya madaraka.

Maofisa hao waandamizi wa TBA; Makumba Kimweri (Mtendaji Mkuu), na Richard Maliyaga (Msanifu Mkuu), walifikishwa mahakamani hapo jana na kusomewa mashitaka yanayowakabili na Wakili wa Serikali, Leonard Swai, mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama hiyo, Sundi Fimbo.

Swai alidai mahakamani hapo kuwa Agosti 6, 2007 Kimweri akiwa Mtendaji Mkuu wa TBA kwa kutumia vibaya madaraka yake, alisaini hati ya makubaliano yenye namba TBA/JVA/DSM/ROI/001 kati ya TBA na Kampuni ya Royalle Orchard Inn Ltd akiwa na lengo la kuanzisha ujenzi na wamiliki binafsi wa umma wa ghorofa 15, kwenye Kitalu namba 45 katika Mtaa wa Chimara, Wilaya ya Ilala bila eneo hilo kufanyiwa upembuzi yakinifu.

Alidai pia kuwa katika tarehe hiyo hiyo, Kimweri alitumia vibaya madaraka kwa kusaini hati ya makubaliano namba TBA/JVA/DSM/ROI/002 kati ya TBA na kampuni hizo akiwa na lengo la kuingia ubia kati serikali na kampuni binafsi (PPP) wa ghorofa 15, kwenye Kitalu namba 46 eneo la Chimara bila kufanya upembuzi yakinifu katika mradi huo na kuipatia faida Kampuni ya Royalle Orchard Inn Ltd.


Swai alidai kuwa Julai 21, 2008, mshitakiwa Richard, ambaye ni Msanifu Mkuu kwa kutumia vibaya madaraka yake, alitoa hati namba TBA/BP/155 na kuruhusu Kampuni ya Royalle Orchard Inn Ltd kujenga ghorofa 15 za biashara kwenye Kitalu namba 45 na 46 bila ridhaa ya Mipango Miji ya Manispaa ya Ilala na kuipatia faida kampuni hiyo.

Pia alidai kuwa Aprili 9, 2009, Richard kwa kutumia madaraka yake vibaya, aliruhusu Kampuni ya Royalle Orchard Inn Ltd kujenga ghorofa 15 hadi 18 za biashara katika Mtaa wa Chimara, Kitalu cha 45 na 46 bila ridhaa husika ya Mipango Miji ya Manispaa ya Ilala na kuipatia kampuni hiyo faida.

Katika shtaka la mwisho, washtakiwa wote kwa pamoja walidaiwa kuwa katika tarehe tofauti katika ofisi za TBA; Kimweri akiwa Mtendaji Mkuu na Richard akiwa Msanifu Mkuu, katika utekelezaji wa kazi zao, walitumia vibaya madaraka kwa kuiruhusu Kampuni ya Royalle Orchard Inn Ltd kujenga jengo la biashara kwenye Kitalu namba 45 na 46 katika Mtaa wa Chimara, Wilaya ya Ilala, jijini Dar es Salaam bila kupata ruhusa kwa ajili ya mabadiliko ya matumizi ya ardhi kutoka kwa mamlaka husika na kuipatia faida kampuni hiyo.

Wakili Swai alidai kuwa hakuna pingamizi la dhamana ila mahakama izingatie kuwa thamani ya jengo haijatajwa ila ni zaidi ya Sh. milioni 100 na kwamba, upelelezi wa shauri hilo umekamilika.

Hakimu Fimbo alitoa masharti ya dhamana kwa kila mshitakiwa kuwa na wadhamini watatu watakaosaini bondi ya Sh. milioni 50 kila mmoja.

Kesi hiyo iliahirishwa hadi Agosti mosi, mwaka huu, washitakiwa watakapoenda kwa ajili ya kusomewa maelezo ya awali.

CHANZO: NIPASHE
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...