Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Ernest Mangu.
FAMILIA moja ya watu wanne, akiwemo bi harusi mtarajiwa, Bushrati
Bushiri (23) aliyetarajia kufunga ndoa Julai 13, mwaka huu, wamepoteza
maisha baada ya nyumba walimokuwa wamelala kuteketea kwa moto.
Tukio hilo la kusikitisha lilitokea saa 6:00 usiku wa Julai 10, mwaka
huu eneo la Lumala, Kata ya Pasiansi, Manispaa ya Ilemela, jijini hapa
ikiwa ni siku mbili tu kabla ya ndoa ya Bushrati.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Naibu Kamishna wa Polisi
(DCP) Ernest Mangu, nyumba iliyoteketea kwa moto ni ya Nuru Fadhili
(46) mkazi wa Lumala, Pasiansi.
Mbali na Bushrati, Kamanda Mangu aliwataja marehemu wengine waliotokana
na moto huo uliotokea usiku kuwa ni Amina Musa (75), Mariam Musa (72) na
mtoto Janetha Abdul ambaye umri wake haukujulikana mara moja.
Alisema mwanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Kiseke, Doto Twaha (17)
alinusurika katika ajali hiyo kwa kupata majeraha mwilini na amelazwa
katika Hospitali ya Rufaa Bugando (BMC) akipata matibabu.
Kamanda Mangu alisema chanzo cha moto huo ni jiko la mkaa ambalo
lilikuwa sebuleni kwa ajili ya kupasha chakula cha mwezi mtukufu (daku)
usiku.
Alisema kwamba mkaa ulidondokea kwenye zulia kisha kushika masofa na
pikipiki iliyokuwa imeegeshwa sebuleni na kusambaa nyumba nzima huku
marehemu wakiwa usingizini.