Kwa ufupi
Hatua inayofuata sasa ni mijadala ya rasimu hiyo
katika Mabaraza ya Katiba itakayojadili mapendekezo ya tume hiyo, ambayo
sisi wa Mwananchi tunadhani ni mapendekezo mazuri yatakayoipatia nchi
yetu Katiba bora.
Tume ya Mabadiliko ya Katiba jana katika tukio
la kihistoria ilizindua rasimu ya Katiba Mpya itakayojadiliwa na
Mabaraza ya Katiba kabla ya wananchi kupiga kura ya maoni kuikataa au
kuikubali rasimu hiyo. Iwapo wananchi watapitisha rasimu hiyo, Bunge la
Katiba litakaloundwa na wabunge wa Bunge la Muungano, wajumbe wa Baraza
la Wawakilishi na wajumbe watakaoteuliwa na Rais wa Jamhuri litakaa na
kupitisha Katiba Mpya.
Rasimu hiyo ya Katiba Mpya iliyozinduliwa jana na
Mwenyekiti wa Tume hiyo, Jaji mstaafu Joseph Warioba ilizingatia maoni
yaliyotolewa na wananchi wakati wa mchakato wa kukusanya maoni. Kazi
kubwa ya wajumbe wa Tume hiyo ilikuwa ni kuzunguka nchi nzima, ambapo
maoni ya watu 1,015,564 yalikusanywa kwa njia mbalimbali ikiwa ni pamoja
na waliohudhuria mikutano ya moja kwa moja, waliotuma ujumbe mfupi wa
simu (sms), barua pepe na kutumia mitandao ya kijamii.
Rasimu hiyo ina mapendekezo ya Tume kuhusu masuala
mbalimbali ambayo wananchi walitaka yaingizwe katika Katiba Mpya. Kama
tulivyosema hapo juu, rasimu hiyo imepatikana baada ya Tume hiyo
kuchambua kwa kina maoni hayo yaliyotolewa na wananchi kwa njia
mbalimbali. Bila shaka haikuwa rahisi kwa Tume kufanya uchambuzi wa
maoni hayo kutokana na ukweli kwamba baadhi ya maoni kuhusu masuala
nyeti ya kitaifa yalikuwa yakikinzana, hivyo Tume ilibidi ifanye uamuzi
mgumu wa kuainisha maoni hayo na kutoa mapendekezo kwa kuzingatia wakati
tuliomo, uzoefu wa mataifa mbalimbali na masilahi ya taifa letu.
Hatua inayofuata sasa ni mijadala ya rasimu hiyo
katika Mabaraza ya Katiba itakayojadili mapendekezo ya tume hiyo, ambayo
sisi wa Mwananchi tunadhani ni mapendekezo mazuri yatakayoipatia nchi
yetu Katiba bora. Tangu kuanza kwa mchakato wa kupata Katiba Mpya
tumekuwa tukiwaomba wananchi kupitia safu hii kutoa ushirikiano kwa Tume
hiyo, tukisisitiza kwamba Tume hiyo imeundwa na wajumbe wenye uadilifu
mkubwa na wenye rekodi ya utumishi uliotukuka. Tulisema wajumbe hao wako
juu ya udini na itikadi za kisiasa, hivyo wangezingatia tu matakwa na
masilahi ya taifa katika kufanya kazi yao.
Tulifarijika jana kuona Tume hiyo ikizindua rasimu
yenye mapendekezo ya kuleta utengamano badala ya utengano katika taifa
letu. Ni mapendekezo ya kuboresha hali ya Muungano, umoja, amani, haki
za binadamu, demokrasia, utawala bora na kadhalika.
Ni mapendekezo yanayoruhusu mabadiliko katika
mfumo wa utawala, muundo wa Muungano, Bunge, Serikali, Mahakama na
ushiriki wa wananchi katika uongozi wa nchi, ikiwa ni pamoja na haki ya
kila mtu kugombea nafasi ya uongozi kuanzia ngazi ya chini hadi urais.
Kwa maneno mengine, mgombea binafsi sasa ruksa.
Tume pia imependekeza kuwapo serikali tatu.
Madaraka ya rais yapunguzwe kama ilivyo kwa mambo yanayohusu Muungano
ambayo sasa imependekezwa yabakie saba tu. Imependekezwa uwepo ukomo wa
ubunge na Viti Maalumu vifutwe. Yapo pia mapendekezo kuhusu muundo wa
Tume ya Uchaguzi, Msajili wa Vyama vya Siasa, mawaziri kutokuwa wabunge
na mapendekezo mengine mengi.
Ni matumaini yetu kwamba Mabaraza ya Katiba
yataepuka udini na itikadi za kisiasa katika kujadili mapendekezo hayo.
Ni matumaini yetu pia kwamba katika mchakato mzima wa kupata Katiba Mpya
hakuna mwananchi atakayepoteza, wananchi wote wataibuka washindi.
E&P
Chanzo: Mwananchi
Chanzo: Mwananchi