Dar es Salaam. Juma lilipopita, tuliandika makala ambayo
majeruhi walieleza jinsi ambavyo bomu hilo lilitupwa mpaka kutua chini
na baadaye kulipuka. Fatma Tarimo (39), Mkazi wa Olasiti mkoani Arusha,
anaendelea kusimulia mkasa wa bomu hilo. Endelea...
Alivyoumia
Mpaka Mwananchi inafanya mazungumzo na mama huyo
katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) ambako amelazwa, tayari
alikuwa amefanyiwa upasuaji mara tatu ili kutolewa vyuma kwenye maeneo
mbalimbali ya mwili wake.
“Mpaka sasa hivi nimetolewa vyuma vitatu, kwanza
kilikuwa cha mviringo, kingine kama msumari, na kingine kilikuwa na umbo
lilokaribia kuwa duara, nimeumia sana kwenye maeneo ya upande wa kulia
kuanzia kwenye mguu, mbavu na mapafu,” anasema.
Chuma kwenye mapafu hakiwezi kutoka
Anasema mbali na upasuaji huo aliofanyiwa, kuna
chuma ambacho kipo kwenye mapafu na amebainisha kwamba madaktari
wamemwambia hakiwezi kutolewa.
“Madaktari wanasema kuna chuma kidogo kwenye
mapafu, lakini wanasema hakina madhara na hakiwezi kutoka kwa sababu
kipo karibu na sehemu ya hewa,” anasema.
Anaeleza kuwa, alipokuwa katika Hospitali ya Mkoa
wa Arusha ya Mount Meru, alifanyiwa operesheni ambayo chuma kingine
kilitolewa kwenye mapafu.
“Kwa sasa hivi madaktari wanasema vidonda vingine
vitapona tu, kwakweli wametuhudumia sana. Kwa upande wa maumivu yapo
kwenye mapafu,” anasema.
Bomu lilimgonga begani
Mtu mwingine aliyeumia kwenye tukio hilo ni Jenifa Joachim (34) na anasema kwamba bomu hilo lilimgonga begani na kutua chini.
“Nilidhani ni jiwe limerushwa na watoto, nilikuwa
nimemshika mkono mtoto wangu kwa hiyo nikaendelea kufuatilia ibada wala
sikuangalia lilipoangukia.
“Baada ya muda kidogo nilisikia kishindo kikubwa, nikasikia miguu inauma, ule moshi ulijaa mdomoni nikashindwa hata kuzungumza.
“Baada ya kike kishindo, nilisikia miguu inauma,
sikuweza kukimbia nikawa nimekaa chini, kwa mbali nikaona mtoto wangu
anatoa macho nikajua amekufa, sikuweza kumfuata wala kuomba watu
wamsaidie kwa kuwa sikuweza kuzungumza wala kunyanyuka,” anasema.
Anasema hivi sasa mtoto wake amelazwa katika Hospitali ya KCMC mkoani Kilimanjaro.
“Sijamwona wala kuzungumza naye mpaka sasa, naambiwa tu kwamba ameumia sehemu ya kichwa, bega na mguu,” anafafanua.
Anaeleza kwamba kwa kawaida mwanaye huyo anakwenda
kwenye ibada ya kwanza na kwamba siku hiyo alilazimika kwenda naye kwa
sababu kulikuwa na misa moja tu.
“Kwa wiki nzima nilikuwa nimeipania hiyo siku, nilikuwa nimepanga kwa vyovyote siwezi kuikosa.
“Sikutegemea kama kuna kitu kama hicho kinaweza
kutokea, wakati nikiwa chini nilishtuka nikasema labda ni mwisho wa
dunia, kwa sababu niliona watu wameanguka wanatoka damu kila mahali,
nikashtuka kweli,”anasema.