Blogger Widgets

Social Icons

Pages

Friday, June 7, 2013

Kamati Kuu CCM kukutana kujadili Rasimu ya Katiba

. 
HATUA ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba kutangaza rasimu ya Katiba mpya siku chache zilizopita, imeibua fukuto jipya la kisiasa lenye mwelekeo wa kuipinga. 


Tayari baadhi ya wanasiasa kutoka vyama mbalimbali hususan wale wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), wamekwishakaririwa wakieleza kutokubaliana nayo kwa madai kuwa haiendani na mfumo wa siasa za kileo na kwamba imelenga kuongeza mzigo wa uendeshaji wa Serikali.
Mbali na wanasiasa mmoja mmoja, waliokwishatoa maoni yao yenye mwelekeo wa kutokubaliana na baadhi ya vipengele katika rasimu hiyo, CCM kimetangaza kuitisha kikao cha dharura cha Kamati Kuu (CC) kwa ajili ya kuijadili.
Tangazo la kuitishwa kwa CC ya CCM, lilitolewa mjini Dar es Salaam jana na Katibu Mkuu wake, Abdulrahaman Kinana, mbele ya waandishi wa habari ambaye alieleza kuwa itakutana Jumatatu ya wiki ijayo, kwa ajenda moja tu ya kupitia kwa undani rasimu ya Katiba mpya.
Taarifa kutoka vyanzo vya ndani ya chama hicho, zimeeleza kuwa mjadala unatarajiwa kuwa mkali wakati wa kujadili suala la Serikali tatu, ambalo tangu kutangazwa kwa rasimu hiyo ikipendekeza hivyo, baadhi ya vigogo waliokwishatangaza au kuonyesha nia ya kuwania urais wamekuwa katika sintofahamu ya nini cha kufanya.
Ni sintofahamu hiyo, inayoonekana kukikumba pia CCM ambacho kupitia kwa Kinana kimeeleza kuwa CC itakayoketi Jumatatu, itaangalia kwa undani iwapo rasimu ya Katiba mpya, itakidhi matakwa halisi ya wakati huu.
“Siwezi kuzungumzia msimamo wa chama kuhusu rasimu hiyo kwa sasa hadi Kamati Kuu ya chama, itakapokuwa imekaa Jumatatu ijayo.
“Si busara kuharakisha kuzungumzia suala hilo kabla chama hakijakaa na kuichambua kipengele kwa kipengele, kuona kama inakidhi hali halisi ya matakwa ya kisiasa tuliyo nayo sasa,” alisema Kinana.-Wakati Kinana akieleza hayo, duru za kisiasa kutoka ndani ya CCM, zinaeleza kuwa Rasimu ya Katiba mpya imeibua hali na wasiwasi kwa vigogo wa chama hicho wanaohofia chama chao kupoteza nguvu za mamlaka ya dola kutokana na upepo wa kisiasa unavyovuma sasa nchini.
Wadadisi na wafuatiliaji wa mambo walio ndani ya CCM, wanaeleza iwapo muundo wa Serikali tatu za Zanzibar, ya Tanzania Bara na ile ya Jamhuri ya Muungano kama zilizopendekezwa na Tume ya mabadiliko ya Katiba utaridhiwa, CCM kinaweza kuambulia ukuu wa Serikali ya Muungano pekee.

Imani hii ya wadadisi na wafuatiliaji wa mambo, inajengwa katika msingi wa uungwaji mkono na wananchi kwa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kwa upande wa Tanzania Bara na Chama cha Wananchi (CUF) kwa upande wa Zanzibar.

Kwa msingi huo, haina shaka kuwa CUF ambacho kina nguvu kubwa ya kisiasa kwa upande wa Zanzibar, kinaweza kuibuka kidedea katika kinyang’anyiro cha urais, huku Chadema kinachoendelea kujipatia umaarufu na uungwaji mkono mkubwa wa wananchi kikichukua udhibiti wa Serikali ya Tanzania Bara na kukiacha CCM kikibaki na udhibiti wa Serikali ya Muungano ambayo kinaweza kushinda kutokana na historia yake ya kusaka ushindi wa jumla.-

Wakati wadadisi na wafuatiliaji wa mambo wakitoa tathimini hiyo kwa upande wa vyama, wachambuzi wa siasa za ndani ya CCM wameeleza kuwa, iwapo chama hicho kitapoteza nguvu ya udhibiti za Serikali za Tanzania Bara na ile ya Zanzibar na kubaki na Serikali ya Muungano pekee, hilo linaweza kuwa anguko lake la kiuchumi.

Inaelezwa CCM kikiwa na udhibiti wa Serikali ya Muungano, hakitakuwa na ardhi ambayo kimekuwa kikiitegemea zaidi kwa ajili ya kujiendesha kiuchumi jambo ambalo litakifanya kitegemee zaidi misaada ya wahisani.

Baadhi ya wataalamu wa uchumi, waliozungumza na gazeti hili kwa sharti la majina yao kuhifadhiwa kuhusiana na mwenendo huo wa mambo, walieleza kuwa CCM kikiwa na udhibiti wa Serikali ya Muungano, hakitaweza kujiendesha na pia kitashindwa kuwahudumia wananchi kwa sababu kitakuwa tegemezi kwa wafadhili kama vilivyo vyama vya upinzani hivi sasa.Vyama vitavyonufaika na mfumo mpya wa uundwaji wa Serikali kama ilivyopendekezwa kwenye rasimu, ni kile ambacho kitakuwa na udhibiti wa dola ya Zanzibar, ambacho kitadhibiti ardhi, rasilimali na uchumi wa jumla na kile ambacho kitashika dola Tanzania Bara ambacho pia kitakuwa na ardhi na kumiliki rasilimali za nchi.

Mambo haya ndiyo yanayoonekana kuwaumiza vichwa wanasiasa na vyama ambavyo vimekuwa vikipambana kuwania ukuu wa dola, ambapo tangu Juni 3, siku ambayo Jaji Joseph Warioba, alitangaza rasimu ya Katiba mpya iliyokuwa ikipendekeza kuwepo kwa muundo wa Serikali tatu, fukuto la kisiasa kwa wanasiasa walioonyesha tamaa ya urais na vyama vinavyoiwinda Ikulu, limepanda.Ndani ya CCM, kuna vigogo kadhaa ambao wameonyesha nia ya kugombea urais mwaka 2015, ambao Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa, Waziri wa Ujenzi, John Magufuli, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano), Stephen Wassira, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernad Membe na Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta.

Kwa upande wa Chadema, watu ambao wanatajwa kuonyesha nia ya kugombea urais ni Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk. Willbrod Slaa, Naibu Katibu Mkuu, Kabwe Zitto na Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe.

Lakini Chama cha Wananchi (CUF) nacho hakiko nyuma, kwani Mwenyekiti wake, Profesa Ibrahim Lipumba amekwisha tangaza nia ya kugombea urais kwa mara ya nne mwaka 2015.
 
Credit: audifacejackson.blogspot.com

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...