Blogger Widgets

Social Icons

Pages

Monday, June 17, 2013

DPP ataka Lwakatare arudi rumande


MKURUGENZI wa Mashtaka nchini (DPP), amewasilisha kusudio la kukata rufaa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam kupinga Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Wilfred Lwakatare kuwa nje kwa dhamana. DPP aliwasilisha kusudio hilo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu mwishoni mwa wiki, baada ya mahakama hiyo kumwachia Lwakatare kwa dhamana Juni 11 mwaka huu.

Lwakatare na Ludovick Joseph walikubaliwa kupata dhamana mbele ya Hakimu Mkazi Aloyce Katemana kwa masharti ya kuwa na wadhamini wawili wa kuaminika, wanaotoka katika taasisi zinazotambulika kisheria ambao kila mmoja wao atasaini dhamana ya Sh milioni 10 pamoja na washtakiwa wenyewe. 

Hakimu Katemana aliwataka washtakiwa hao kusalimisha hati zao za kusafiria mahakamani na hawataruhusiwa kuwa nje ya Dar es Salaam bila ya kuwa na kibali cha mahakama. Ludovick alishindwa kutimiza masharti yuko rumande.

“Mshtakiwa wa kwanza ametimiza masharti ya dhamana, hivyo atakuwa nje kwa dhamana hadi Juni 24 mwaka huu na ahakikishe anafika mahakamani kila kesi inapotajwa.

“Mshtakiwa wa pili utaendelea kuwepo rumande hadi utakapokamilisha masharti ya dhamana wakati wowote,” hayo yalikuwa maneno ya Hakimu Katemana siku alipokubali kuwapa dhamana washtakiwa hao.

Lwakatale na Ludovick walikubaliwa dhamana baada kufutiwa mashtaka matatu ya ugaidi na Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam na kubakiwa na shtaka moja la kula njama ya kumdhuru kwa sumu Dennis Msacky.

Katemana baada ya kupitia hoja za kuomba dhamana zilizotolewa na Wakili Peter Kibatala alikubali kuwapa dhamana washtakiwa hao, kwa sababu shtaka linalowakabili lina dhamana kisheria.


habari NA KULWA MZEE, DAR ES SALAAM
PICHA - CHINGAONE BLO LIBRARY
chanzo - mtanzania
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...