Rais
Kikwete akiambatana na Mama Salma Kikwete na ujumbe wake ameondoka
nchini mchana wa jana, Jumapili, Aprili 14, kwenda Uholanzi tayari kwa
ziara hiyo ambako pia ataandamana na Mawaziri wanne wa Serikali.
Mawaziri
hao ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Mheshimiwa
Bernard Membe, Waziri wa Viwanda na Biashara Mheshimiwa Dr. Abdallah
Kigoda, Waziri wa Nishati na Madini Mheshimiwa Profesa Sospeter Muhongo
na Waziri wa Maji, Ardhi, Nishati na Maendeleo ya Makazi wa Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar Mheshimiwa Ramadhan Shaaban.
Katika
siku ya kwanza ya ziara yake leo, Rais Kikwete atafanya mazungumzo rasmi
ya Kiserikali kati ya Tanzania na Uholanzi kwenye Makazi Rasmi ya
Waziri Mkuu. Mazungumzo hayo rasmi yatakuwa kati ya Rais Kikwete na
ujumbe wake na Waziri wa Mambo ya Nje wa Uholanzi Mheshimiwa Frans
Timmermans.
Baada ya
mazungumzo hayo rasmi, Rais Kikwete atakutana kwa mazungumzo na HRH
Princes Maxima, Mke wa Mfalme Mtarajiwa wa Uholanzi, Prince of Orange
Willem Alexander ambaye anatarajiwa kurithi kiti cha Ufalme kutoka kwa
Mama yake, Malkia Beatrix, mwishoni mwa mwezi huu, Aprili 30, 2013.
Baadaye,
Rais Kikwete na ujumbe wake atakutana na kufanya mazungumzo na Her
Majesty Malkia Beatrix wa nchi hiyo ambaye anastaafu rasmi Aprili 30
mwaka huu kumwachia nafasi hiyo mwanawe, Prince Willem Alexander.
Miongoni
mwa shughuli zake nyingine za leo, Rais Kikwete atakutana na uongozi wa
Kampuni ya Rijk Zwaan Netherlands Limited, atakula chakula cha mchana
cha kazi na wawakilishi wa Jumuiya ya Biashara ya Uholanzi na baadaye
atakutana kwa mazungumzo na viongozi wa Chama cha Wenye Viwanda na
waajiri wa nchi hiyo.
Kesho,
Jumanne, Rais Kikwete atatembelea Bandari ya Rotterdam, moja ya bandari
maarufu zaidi duniani, atakutana kwa mazungumzo ya faragha kati yake na
Waziri Mkuu wa nchi hiyo, Mheshimiwa Mark Rutte ambaye pia watakula naye
chakula cha mchana.
Mchana,
Rais Kikwete atatembelea Kampuni maarufu ya mafuta duniani ya Shell na
kukutana na jumuiya ya Watanzania wanaoishi Uholanzi.
Rais Kikwete na ujumbe wake anatarajiwa kurejea nchini Jumatano, Aprili 17, 2013.
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu.
Dar es Salaam.